Maiti ya Mbunge wa Emurua Dikir Johana Ng'eno na watu wengine watano waliofariki kwenye ajali ya helikopta huko Mosop, Kaunti ya Nandi, ilihamishwa hadi Makafani ya Lee hapa Nairobi siku ya Jumapili. Awali Miili ya waathiriwa ilikuwa imepelekwa katika Makafani ya hospitali ya Moi, Eldoret saa chache baada ya ajali hiyo ya Jumamosi jioni. Familia, marafiki na viongozi wa kisiasa walioongozwa na waziri wa usalama Kipchumba Murkomen na mwenzake wa usafiri David Chirchir walifika katika Uwanja wa Ndege wa Jomo Kenyatta kupokea miili hiyo, kabla ya msafara wa kuelekea Makafani ya Lee.