Idara ya Mahakama imesema shughuli za mahakama zitaendelea kama kawaida licha ya tisho la Chama cha Wanasheria nchini, LSK, kuwa huduma za mahakama zitatatizwa Jumatano. Idara hiyo imesema itafanya mkutano na LSK mwishoni mwa mwezi huu kutafuta suluhu kwa malalamishi yake kuhusu uwajibikaji mahakamani. Katika taarifa, msemaji wa Idara ya Mahakama, Paul Ndemo, amesema tisho la kususia shughuli za mahakama si njia mwafaka ya kutatua malalamishi ya LSK. Wakati huo huo, Idara ya Mahakama imesema kuwa Tume ya Huduma za Mahakama, JSC, pamoja na Ofisi ya Kusikiza Malalamishi ya Umma, zinaendelea kupokea na kushughulikia malalamishi yaliyowasilishwa.