Utoaji wa huduma za afya umeathirika katika hospitali za umma kaunti ya Laikipia kufuatia mgomo wa wauguzi ulioanza rasmi siku ya Jumatatu na kuhusisha vyama vitano vya wafanyakazi wa sekta hiyo.
Wagonjwa wamelazimika kuondolewa hospitalini huku wale wanaotafuta huduma za nje wakirejeshwa nyumbani kutokana na kusitishwa kwa huduma. Katika hospitali ya rufaa ya Nanyuki, wagonjwa waliokuwa wamelazwa wameondolewa mapema na wengine kupewa rufaa ya kuhamishiwa katika hospitali za kibinafsi. Mazungumzo kati ya serikali ya kaunti ya Laikipia na vyama husika yamegonga mwamba, hali iliyochochea kuendelea kwa mgomo na kulemaza huduma za afya katika hospitali za umma.